TEMESA NDANI YA MAADHIMISHO YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA DODOMA
Posted On: June 20, 2026
Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) unashiriki katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyoanza tarehe 16 Juni, 2026 katika viwanja vya Chinangali Mkoani Dodoma. Maadhimisho hayo yana lengo la kutatua kero na changamoto za kiutumishi kwa wananchi ili kuongeza uwajibikaji na utawala bora.
Wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Dodoma wamekuwa wakifika katika banda la TEMESA kupatiwa elimu kuhusu shughuli mbalimbali zinazofanywa na TEMESA ikiwemo huduma za matengenezo ya magari, kazi za umeme, tehama na elektoniki pamoja na miradi ya ujenzi wa vivuko inayoendelea kutekelezwa Nchini.
Miongoni mwa wageni waliotembelea banda la TEMESA katika maonesho hayo ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya mji Arusha Bwa. Suleyman Msumi ambapo akiwa katika banda hilo aliipongeza TEMESA kwa kuanzisha mifumo ya kidigitali ya kazi za matengenezo ambapo amesema mifumo hiyo imewawezesha kupata urahisi wakati wa kuomba kazi za magari, umeme na elektroniki kwakuwa imepunguza muda na kuepusha mlolongo wakati wa kuomba huduma ya matengenezo. Bwa. Msumi pia ameshauri wataalamu wanaosimamia mitambo na magari makubwa kupatiwa mafunzo ya mara kwa mara ili kuwawezesha kutoa huduma bora na kwa weledi.
Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yenye kauli mbiu, '' Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu'', yameanza tarehe 16 Juni na kufunguliwa rasmi tarehe 17 Juni, 2026 na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete na yanatarajiwa kufungwa tarehe 23 Juni, 2026..