WAZIRI KAPINGA AIPONGEZA TEMESA KWA KUPIGA HATUA KUBWA YA UTOAJI HUDUMA KIDIGITALI

News Image

Posted On: July 02, 2026

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga ameupongeza Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kutengeneza magari pamoja na huduma mbalimbali wanazotoa kupitia vyombo vya moto vilivyopo chini yake na kusisitiza kuwa taasisi hiyo imepiga hatua kwakuwa inaenda na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

Mheshimiwa Kapinga ametoa kauli hiyo Julai Mosi alipotembelea banda la TEMESA katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (DITF) maarufu kama Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

Waziri Mhe. Kapinga amesema kwa niaba ya Serikali anaipongeza TEMESA kwa kasi ya mabadiliko inayoenda nayo katika matengenezo ya magari na mabadiliko ya mifumo ya utoaji huduma.

“Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnazozifanya katika matengenezo ya magari na pia matumizi yenu ya mifumo katika utoaji huduma,hongereni sana,”amesema Mhe. Kapinga.

Akiwa katika banda hilo, Waziri Kapinga alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na TEMESA, ikiwemo huduma za vivuko, umeme na elektroniki, matengenezo ya magari na mitambo, ushauri wa kihandisi pamoja na mifumo ya kidijitali na ubunifu unaolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

TEMESA inaendelea kuwakaribisha wananchi, wadau na wageni wote kutembelea banda lake ili kujifunza kuhusu huduma zake, kupata ushauri wa kitaalamu na kufahamu mchango wa TEMESA katika maendeleo ya sekta ya ufundi na umeme nchini.

Maonesho ya 50 ya biashara yanatarajiwa kufunguliwa rasmi kesho Julai 3 na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji Daniel Chapo ambapo ataambatana na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan.

Maonesho hayo ya biashara yamebebwa na kauli mbiu isemayo “Hii ni Kubwa Kuliko” na yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi siku ya ijumaa tarehe 3 Juni, 2026